MENU

Where the world comes to study the Bible

Mwongozo Wa Kujifunza Kukua Kiroho: Maombi

Related Media

I. Mwendelezo Mpya: Ni Nini Kinahitajika Ili Mtu Akue? Ni Maombi.

Tulianza mwendelezo mpya juma lililopita juu ya swali hili, “Ni nini kinahitajika ili mtu akue?

Tuliona kwamba kuijua na kuitii Biblia hakuna mjadala kwamba ni muhimu sana ikiwa unataka kukua hadi kufikia kuwa Mkristo aliyekomaa.

Ni matumaini yangu kwamba uliangalia orodha ya mapendekezo yaliyotolewa ili kukusaidia kubobea katika eneo la kujifunza Biblia kwa ufanisi. Natumaini pia kwamba ulichagua nafasi mmojawapo na kuhakikisha kuwa unajitahidi kuweka moyoni kwa wingi Neno la Mungu juma hili na mwezi huu.

A. Shabaha: Ujenge Tabia Zinazohitajika Ili Kukomaa Kiroho

Aya ya Ujumbe: 2 Pet. 3:18 Lakini kueni katika neema na katika kumjua Bwana wetu na Mwokozi Yesu Kristo. Utukufu una yeye sasa na hata milele. Amina.

Je, uliwahi kutambua kuwa Mungu anataka ukue? Mungu haridhiki kwamba umempokea Yesu Kristo kama Mwokozi, anataka sasa umfuate na kumtii kama Bwana wa maisha yako. Umtii yeye.

B. Kukomaa Kiroho Huwa Kunachukua Muda Gani?

Je, maandiko yana dokezo lolote la kuonyesha kuwa inachukua muda gani hadi tuambiwe kuwa “tumekomaa”? Naam. Dokezo lipo. Paulo aliandika barua kwa 1 Wakorintho miaka minne hadi mitano baada ya kuwa ametoa huduma katika mji wa Korintho. Huenda alifika pale mwaka 51 A.D. na akakaa pale hadi mwaka 53 A.D. aliandika waraka wa 1 Wakorintho kama mwaka 56 – 57 A.D. Alitarajia kwamba miaka 4 – 5 ingetosha kwa Wakorintho kuwa wamefikia kiwango cha kukomaa.

Hapa ndivyo anavyosema katika 1 Wakorintho 3:

1Lakini ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. 2Naliwanywesha maziwa, sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi, 3kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu? Mnaishi kana kwamba ninyi sio watu wa Bwana. Kama umekuwa Mkristo kwa chini ya miaka mitano, usiharakishe kukomaa lakini unaweza kujitahidi kukua kawaida tu.

Da! Miaka mitano! Je hili linakufanya ujisikie vibaya? Labda umekuwa Mkristo kwa zaidi ya miaka 5. Unafahamu kwamba ulipaswa kuwa mbali kuliko mahali uliko sasa, lakini unaifariji dhamiri yako kwa kusema, “Nadhani naendelea vizuri na siku moja nitakuwa mkomavu na hakuna ajuaye kuwa ni lini.” Kukomaa kiroho sio lengo lililoko mbali na la kufikirika ambalo huwezi kulifikia au utalifikia mwezi mmoja kabla ya kufa. Kwa mujibu wa Paulo kukomaa ni shabaha ya kawaida na nyeti ambayo unaweza kuifikia kwa muda ambao ni mfupi. Wewe unaendeleaje kiroho?

C. Mapitio Ya Tabia Saba Za Mkristo Anayekomaa

Hapa tunaangalia Tabia Saba za Msingi ambazo kila Mkristo anahitaji kuwa nazo ili aweze kukua hadi kukomaa. Tutakachofanya hapa ni…

  • Kukupa stadi unazozihitaji ili kuanza tabia hizi.
  • Kuelezea zana unazozihitaji ili kuendeleza tabia hizi.
  1. Ili Uweze Kukua Unahitaji Kula – Biblia
  2. Ili Uweze Kukua Unahitaji Kupumua – Maombi
  3. Ili Uweze Kukua Unahitaji Usafi Wa Kiroho –Kuungama Dhambi
  4. Ili Uweze Kukua Unahitaji Familia Inayojali – Ushirika
  5. Ili Uweze Kukua Kupata Mazoezi Kila Mara – Huduma
  6. Ili Uweze Kukua Unahitaji Ulinzi – Majaribu
  7. Ili Uweze Kukua Unahitaji Kutoa – Uwakili

Tabia Ya Maombi

“Iwekeni furaha yenu katika Tumaini lenu katika Kristo. Majaribu yakija, myastahimili kwa uvumilivu; mkidumisha tabia ya maombi.” Warumi 12:12 (Imetafsiriwa)

II. Je Wewe Uko Sehemu Gani Katika Ukuaji Wako Wa Maombi?

A. Uombaji Wa Mazoea

Kuomba wakati wa kula, Wakati wa kulala. Wakati unapolazimika. Wakati unapotarajiwa kuomba. Hii sio mbaya lakini maombi yanakuwa ni mazoea tu na tena ni ya haraka.

B. Maombi Ya Kujitoa

Haya ni maombi ambayo mwombaji amedhamiria na ana malengo maalum. Unakuwa makini kuhusu kuomba kwako kwa sababu kuna mzigo moyoni mwako unaokufanya upige magoti na kuomba. Hii ni aina ya maombi unayoomba wakati kijana wako anafanya mitihani wa kupata cheti.

C. Maombi Ya VIta

Hapa ndipo Paulo anamzungumzia mtenda-kazi mwenzake,

Wakolosai 4:12 Epafra, aliye mtu wa kwenu, mtumwa wa Yesu Kristo, awasalimu, akifanya bidii siku zote kwa ajili yenu katika maombi yake, ili kwamba msimamo wakamilifu na kuthibitika sana katika mapenzi yote ya Mungu.

Epafra alipigana vita katika maombi kwa ajili ya Wakristo wa Kolosai. Hapa kuna mzigo wa maombi na bidii kubwa. Aina hii ya maombi ni yale maombi ambayo baba huwa anayofanya anaposikia kuwa binti yake amemwacha Mungu, na anaishi kinyumba na mvulana. Hii ni aina ya maombi ambayo mama huwa anayofanya anaposikia kuwa kijana wake amejiunga na kanisa la Mashetani ili aweze kumwoa msichana mrembo kutoka kwenye kanisa hilo.

Katika aina hizi wewe je uko wapi? Uko kwenye ngazi gani katika maisha yako ya maombi?

Je tnawezaje kushinda matatizo yanayovikumba vikundi vya maombi?

III. Jifunze Na Kutumia Vipengele Sita Vya Maombi Yenye Tija.

Hii inatoka katika Mathayo 6:9 – 15, ambayo hujulikana kama Sala ya Bwana. Katika maombi haya Yesu alisema, “Basi ninyi salini hivi” sio kwamba haya ndio mambo ya kuombea. Anatoa kielelezo cha mambo tutakayokuwa tunayatumia wakati wa maombi.

Kuna Vipengele Sita Muhimu vya Maombi yenye Tija

A. Kipengele Cha Kwanza Muhimu Cha Maombi Yenye Tija Ni Sifa. Unaanza Kwa Kuelezea Upendo Wako Kwa Mungu

Baba Yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe (m. 9)

Unapoanza maombi ungependa kuanza kwa kuuelezea upendo wako kwa Mungu. Anza kumwambia, “Bwana, nataka nikutazame Wewe.” Nikaingia kwenye maombi huku nikijiangalia mimi na mahitaji yangu kwanza, nitamaliza maombi yangu nikiwa nimechoka moyoni na kukata tamaa kuliko wakati nilipoanza. Lakini kama nikija kwenye maombi nikiwa namtazama Mungu, nitakachokiona kwake, nitakachojifunza kwake, anachoweza kunionyesha, ndipo badala ya kuondoka hapo nikiwaza jinsi matatizo yangu yalivyo, nitaondoka nikiwaza jinsi Mungu wangu alivyo mkubwa!

Je, unamsifuje Mungu?

1. Kwanza, Unaweza Kumsifu Kwa Jinsi Alivyo – Tabia Yake

Kipengele cha kwanza muhimu katika maombi ni tabia ya Mungu. Tabia ya Mungu ndio msingi wa maombi yanayojibiwa. Mungu hujibu maombi yanayotambua kuwa yeye ni nani.

Wiki iliyopita nilipoteza kifaa changu cha kuandikia. Yaani ilikuwa ni sawa na kuipoteza akili yangu. Nilijaribu kukitafuta kila mahali ndani ya nyumba hadi nikamtuhumu mke wangu kwamba amekichukua. Nilikitafuta sana kila mahali lakini wapi! Sikuona kitu. Nilijaribu kwenda ofisini na kupindua kila kitu lakini sikukiona. Nilisimama kando ya dawati langu la ofisi nikaomba, Ee Mungu, wewe unajua kilipo. Kwa kweli mimi sijui. Nakusihi sana Ee Bwana unisaidie! Niliinama na kufunika Biblia na tazama! Hiki hapa kifaa! Kilikuwa chini ya Biblia niliyokuwa nimeifungua.

2. Pili, Unaweza Kumsifu Kwa Yale Anayoyatenda – Matendo Yake

Zaburi zote zimejikita katika jambo hili – yaani kumsifu Mungu kwa matendo yake ya ajabu kwa watu wake. Je unatunza kumbukumbu ya jambo hili katika maisha yako? Maisha ya familia yako? Ukombozi wa Mungu? Maombi Mungu aliyoyajibu?

Ijumaa hii iliyopita nilimwomba Mungu anisaidie katika mambo mawili mahsusi. Redio kaseti yangu ilipasuka. Hili halionekani kama ni jambo kubwa, na kwa kweli sio kubwa, lakini kila asubuhi wakati nanyoa ndevu na kuoga, huwa nasikiliza kitabu cha Mithali katika redio kaseti yangu. Nilihitaji kutafuta nyingine ambayo ni ya bei nafuu. Jambo jingine ni kwamba, kwa kama miaka 20 iliyopita Nilikuwa na viatu vizuri vya kupanda milima. Kipindi hiki cha baridi niligundua kuwa soli zake zilikuwa zinabanduka. Nilivipeleka kwa fundi na nikaambiwa ingenigharimu dola 65 za Marekani kuvitengeneza. Kwa hiyo nikamwomba Mungu anisaidie kupata viatu vingine vizuri na kwa bei nafuu na redio kaseti nzuri. Hadi kufikia Ijumaa saa nne asubuhi nilipata redio kaseti kwa dola saba na viatu ambavyo vilinikaa vizuri kwa dola 13! Na leo namsifu Mungu kwa kujishughulisha sana na mimi hasa kwa mambo madogo kama haya na akanijibu.

Zaburi 100:4 inasema, “Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru; nyuani mwake kwa kusifu. Mshukuruni, lihimidini jina lake”

  • Nimedhamiria kwamba nitamsifu Mungu kwa yale anayoyafanya.

B. Kipengele Cha Pili Cha Maombi Yenye Tija Ni Kusudi: Jitoe Kikamilifu Kwa Ajili Ya Kusudi La Mungu Katika Maisha Yako

Sehemu inayofuata ya sala ya Bwana inasema,

10Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatimizwe , hapa duniani kama mbinguni

Huku ni kukubali kwamba Mungu ni Mungu na mimi sio. Sehemu hii inanilazimisha kutafakari kama kweli mimi ninataka kusudi la Mungu litimizwe katika maisha yangu, familia yangu, kazini mwangu shuleni kwangu au nchini kwangu.

Je, umewahi kufikiri kwa kina kwamba jambo hili likoje, kumwambia Mungu, “Fanya lolote unanolitaka katika eneo na jambo lolote katika maisha yangu. Nataka yale unayoyataka kuliko yale ninayoyataka.”

Unataka gari jipya. Mungu amekuwa akisema, “Lile la zamani linatosha. Bado linaweza kukusaidia kusafiri toka sehemu moja hadi nyingine, hita inafanya kazi na bima yake iko chini kuilipa. Itunze! Kisha tumia pesa ulizo nazo kusaidia kumaliza kazi yangu kule India kwenye shirika linalohubiri kule Asia.” Hii ndiyo maana hasa ya kuomba kwamba, :Mapenzi yako yatimizwe”.

Unapenda pipi za chocolate. Mungu amekuwa akikuambia, “Achana na pipi za chocolate. Tumia hizo pesa kwenye huduma ya udiakonia.” Hii ndio maana ya kuomba, “Mapenzi yako yafanyike.”

Wewe na rafiki yako wa kike mmekuwa mkifanya ngono. Mmevuka mipaka, lakini hamtaki kuacha hiyo tabia. Mungu amekuwa akisema, “Vunjeni hayo mahusiano. Mnajua wazi kuwa hayo mahusiano yanawaumiza ninyi nyote wawili. Achaneni sasa.”

Hii ndiyo maana ya kuomba, “Mapenzi yako yatimizwe.”

Umekuwa mara nyingi kila ukija nyumbani unatumia muda mwingi kuangalia tamthilia kwenye runinga. Mungu amekuwa akisema, “Familia yako inakuhitaji. Zima hiyo runinga. Punguza muda uangalie masaa matatu tu kwa wiki.”

Hii ndiyo maana ya kuomba, “Mapenzi yako yatimizwe.”

Warumi 12:1 inatuhimiza “Itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai na takatifu ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana.”

  • Dhamira yangu: Nitamtii Mungu kwa lolote atakaloniagiza

C. Kipengele Cha Tatu Kwa Maombi Yenye Tija Ni Mahitaji Yetu: Mwombe Mungu Akupatie Mahitaji Yako.

11Utupe leo riziki yetu

Ni mahitaji gani ninayoyaombea? Kwa kweli ni mahitaji yote. Hakuna jambo kubwa sana kwa Mungu ambalo atalishindwa na hakuna jambo dogo sana kwa Mungu ambalo atalipuuza. Kwa hiyo mahitaji yangu yote nitayaombea.

Kanuni hasa ni hii: mambo yaliyo makubwa yanayokuhangaisha, ndio mambo makubwa kwako kuyaombea. Nakushauri upitie mambo yote yanayokusumbua katika siku uyaandike na uyaweke katika orodha yako ya kuyaombea. Mambo yanayokuhangaisha ndiyo yanayopaswa kuwa mahitaji yako ya kuyaombea.

Wafilipi 4:6 “Msijisumbue kwa neno lolote, bali katika kila neno kwa kusali na kuomba pamoja na kumshukuru, haja zenu zijulikane na Mungu.”

Wafilipi 4:19 inasema “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu.

Maombi ni tangazo langu kwamba namtegemea Mungu. Ninapomwendea ninasema, “Mimi ninakutegemea Wewe tu, Mungu kwa ajili ya mahitaji yangu.”

  • Dhamira: Nitamtegemea Mungu pekee kwa ajili ya mahitaji yangu yote.

D. Kipengele Cha Nne Kwa Maombi Yenye Tija Ni Msamaha: Mwombe Mungu Akusamehe Dhambi Zako.

12Utusamehe dhambi zetu.

Sehemu hii ya sala ya Bwana inasema, Utusamehe deni zetu kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu..”

Kuna hatua nne za msamaha:

A. Mwombe Roho Mtakatifu Afunue Kila Dhambi.

Zaburi 139 inasema “Ee Mungu unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu. Uone kama kuna uovu wowote ndani yangu.”

Mwombe Roho Mtakatifu kufunua dhambi.

B. Ungama Kila Dhambi Kipekee.

Mara nyingine huwa tunaacha kuungama kwa kuamua kusema, “Nisamehe dhambi zangu zote.” Hizo dhambi ulizifanya moja-moja, ni vizuri zaidi kuomba msamaha kwa dhambi moja-moja. Hakuna blanketi la kuzifunika zote.

Mithali 28:13 “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; Bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.”

C. Tengeneza Kwa Wengine Pale Inapobidi

Mathayo 5:23-24 “Ukikumbuka kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.”

Kwa hiyo Mungu akifunua jambo ambalo umemfanyia mtu, nenda katengeneze ili litokee katika dhamiri yako.

D. Pokea Msamaha Wa Mungu Kwa Imani

“Tukiziungama dhambi zetu yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.” I Yoh. 1:9

Dhamira: Nitaungama dhambi zangu kwa Mungu kwa jinsi Mungu anavyozifunua na kuupokea msamaha Wake.

E. Kipengele Muhimu Cha Tano Kwa Maombi Yenye Tija Ni Usafi: Achilia VInyongo Na Uchungu

Sala ya Bwana inasema, “kama sisi nasi tunavyowasamehe waliotutenda dhambi.”

Kristo anachukulia kwamba sisi tutawasamehe wengine kwa sababu sisi nasi tumesamehewa. Mungu hatajibu maombi yako kama utaendelea kuweka vinyongo na uchungu moyoni. Sikiliza kitu Biblia inachosema,

I Yoh 3:21 Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu tuna ujasiri kwa Mungu. Na lolote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake.

Zaburi 66:18 Kama singaliungama dhambi katika moyo wangu, Bwana wangu asingenisikia. Lakini Mungu alisikia! Ametegea sikio maombi yangu.

Dhamira: Nitawaachilia wale walionikosea kwa sababu Mungu amenisamehe.

F. Kipengele Muhimu Cha Sita Kwa Maombi Yenye Tija Ni Ulinzi: Omba Ulinzi Wa Mungu

13Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.

Sisi kama waamini, tunakumbana na vita ya kiroho kila siku na shetani anataka kutushinda kupitia majaribu na hofu. Kama nikiianza siku bila kumwomba Mungu anipe nguvu zake, nitapigana kwa kutumia vile nilivyo navo na haitoshi kitu!

Ukiomba maombi haya unahitaji kupeleleza katika moyo wako na maisha yako ili uone ni wapi unaelekea kuanguka. Unahitaji kujifahamu, kwa sababu Shetani, ambaye ni adui wa nafsi yako, ni mjanja kiasi cha kufahamu madhaifu yetu, na anayatumia ili kutuangusha.

I Kor. 10:13 Lakini kumbukeni kwamba majaribu yanayowapata sio tofauti na yale yanayowapata wengine. Na Mungu ni mwaminifu. Atazuia jaribu lisiwe kubwa kuliko mwezavyo. Mtakapojaribiwa atawaonyesha njia ya kutokea ili lisiwaangushe.

  • Dhamira: Nitajifunza maeneo niliyo na udhaifu na kutegemea ulinzi wa Mungu.

G. Mahusiano

Sala hii inaanza katika mazingira ya mahusiano – Baba Yetu. Kama nikishindwa kuona kwamba nina mahusiano na baba wa mbinguni, maombi yangu yatakuwa yanadhoofu.

Msingi wa maombi yenye tija ni mahusiano na Baba wa Mbinguni mwenye upendo. Mahusiano hushamiri katika mawasiliano na hudhoofika kama mawasiliano hayapo. Sasa Mungu anasikiliza, je wewe unazungumza?

IV. IV. Hitimisho

Kwa dakika 15 zijazo timu ya Kusifu itatuongoza, na tutaenda kutendea kazi kile nilichokuwa nakihubiri. Inaweza ikawa kwamba unapenda kuketi kwenye kiti chako na kuimba huku ukiomba kimya. Hiyo ni sawa kabisa.

Inawezekana uataka kupiga magoti kwenye kiti chako na kuomba. Hiyo pia ni sawa!

Inawezekana kwamba unataka kutoka mbele na uombe pamoja na mzee wa kanisa au mkewe. Watakuwa hapa tayari kukuombea. Wako tayari kukupaka mafuta na kukuombea kama utataka.

Viongozi wetu wa vikundi wapo hapa na watakuwa wanaongoza vikundi vidogo katika kuomba. Kama unapendelea kujiunga na kikundi ili uombe na wengine wachache, chagua kikundi kimoja ujiunge. Sio lazima uombe kwa sauti kubwa. Uko huru kuingia kimya-kimya wakati wengine wakiendelea kuomba.

Basi na tulitendee kazi lile ambalo Bwana Yesu Kristo alilotupa. Tuombe!

Related Topics: Prayer, Teaching the Bible

Report Inappropriate Ad